Wednesday, 20 November 2013

YANGA YAMGOMBANISHA STRAIKA WA MBEYA CITY MWAGANE NA BABA

 
STRAIKA wa Mbeya City, Mwagane Yeya, alitofautiana na baba yake mzazi aitwaye, Yeya Mwanavyembe, kwa muda wa mwezi mmoja alipoifunga Yanga kwenye mechi ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Mwagane alifunga bao hilo kwenye Uwanja Sokoine jijini Mbeya katika mechi iliyomalizika kwa sare ya bao 1-1. Alipofunga alifurahi pamoja na wachezaji wenzake, lakini hali haikuwa shwari kwa mzazi wake huyo ambaye anaipenda Yanga na ni shabiki mkubwa wa klabu hiyo ya Jangwani.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mwagane ambaye alikiri kuwa  alipokuwa mdogo naye alikuwa anaishabikia Yanga akifuata nyayo za baba yake, lakini anasema alipopata akili za utu uzima akazamisha mawazo yake kwa Mbeya City anayoipenda kwa nguvu zote.
“Familia yetu inaipenda Yanga, baba yangu ndiyo haumwambii lolote kuhusu Yanga. Siku ile tulipocheza nao pale Sokine mzee alikasirika kwanini niliwafunga, yaani ulipita kama mwezi mmoja hivi hatukuwa na maelewano mazuri na mzee,” alisema.
“Lakini baadaye nilikaa naye nikamwelewesha, nashukuru Mungu alinielewa na tukayamaliza.”
Mwagane ndiye mchezaji mwanzilishi wa Mbeya City, aliichezea tangu ilipoanzishwa hadi ilipopanda Ligi Kuu.
Mbali ya kucheza, Mwagane pia ni mwalimu wa Shule ya Sekondari Iduda, Uyole na ndiye nahodha wa timu hiyo inayoshiriki ligi hiyo kwa mara ya kwanza lakini imeleta changamoto kubwa.

No comments:

Post a Comment