.

.

SHOP HERE

News
Loading...

.

.

.

shop now

Usajili wa mastraika utakavyotikisa England

 
KUANZIA kwa wasaka ubingwa Chelsea, Arsenal, Liverpool, Everton na Tottenham Hotspur hadi kwa wanaopigania wasishuke daraja West Ham, Fulham, Stoke City na Crystal Palace, makocha wao stori zao zitafanana tu kwenye usajili wa Januari. Wanahitaji mastraika.
Wafungaji ni kitu kinachotingisha kwenye usajili wa Januari wa Ligi Kuu England baada ya klabu zake kuhitaji watu wa namna hiyo kuliko wengine wowote. Jambo hilo ni wazi litawagharimu pesa nyingi ili kunusuru msimu kabla ya kufika Mei.
Mafundi wa kutikisa nyavu kama Gonzalo Higuain, Radamel Falcao, Jordan Rhodes, Diego Costa na wengineo wanatajwa kati ya mastraika watakaotingisha kwa siku 31 za usajili huo zitakapofunguliwa rasmi.
Kocha wa Everton, Roberto Martinez, ambaye alimsajili kwa mkopo Romelu Lukaku katika siku ya mwisho kwenye usajili wa majira ya kiangazi ilikuwa safi kwenye kikosi chake, lakini tatizo lililopo ni kuporomoka kiwango cha straika wake Nikica Jelavic, jambo ambalo litamlazimisha kuingia sokoni ili kusaka mfungaji.
Sam Allardyce wa West Ham ameshaweka wazi kwamba anatarajia kumnasa straika wa Ghana, Asamoah Gyan wakati wa dirisha la usajili la Januari litakapofunguliwa.
Washambuliaji wanaosakwa
Chelsea na Arsenal zinapelekeshana kwenye kusaka ubingwa wa Ligi Kuu England, zote zinahitaji kuwa na straika mmoja wa nguvu na tayari zinagongana kwa Mcolombia, Radamel Falcao, anayekipiga Monaco.
Kocha wa Chelsea, Jose Mourinho amekiri kuumizwa na mastraika waliopo kwenye kikosi chake, Fernando Torres, Samuel Eto’o na Demba Ba, ambao wote watatu wamefunga mabao matano tu kwenye ligi msimu huu. Arsene Wenger wa Arsenal anadhani Olivier Giroud anahitaji kupatiwa mtu wa kushindana naye kwenye safu ya ushambuliaji baada ya sasa kuwa yeye tu, huku Nicklas Bendtner akishindwa kuaminika.
Ukimweka kando Falcao, Mourinho pia anamsaka Gonzalo Higuain wa Napoli, huku Alladyce mipango yake ikiwa ni kumsajili Jermain Defoe wa Tottenham.
Alvaro Morata wa Real Madrid anaziingiza vitani klabu mahasimu wa London, Tottenham na Arsenal, wakati Filip Djordjevic wa Nantes akiwa kwenye rada za klabu ya Hull City na Crystal Palace.
Straika wa zamani wa Sunderland, Asamoah Gyan, anayekipiga Al-Ain kwa sasa anapigiwa hesabu kali na West Ham wakati Mame Biram Diouf, aliyewahi kukipiga Manchester United lakini sasa yupo Hannover anawindwa na Stoke City.
Arsenal inaonekana kusaka straika zaidi, wamemtaja Kostas Mitroglou wa Olympiakos kuwa ni mtu mwingine wanayemhitaji, huku usajili wa staa huyo ukiwaingiza vitani na Liverpool.

Baada ya kumkosa kwenye usajili wa Agosti, Arsenal imepanga kurudi tena kwa Demba Ba wa Chelsea, huku Nikica Jelavic wa Everton akiwindwa na klabu za Tottenham, Hull City na Crystal Palace.
Hawa ni baadhi tu ya mastraika wanaoweza kupatikana kirahisi katika usajili huo wa Januari.
Hali ilivyo
Kutimiza ndoto zake za kucheza Kombe la Dunia mwakani, straika Jelavic ameelezwa na kocha wake Martinez kwamba akubali kutolewa kwa mkopo kwenye usajili wa Januari. Lakini, tayari Everton itakuwa na upungufu wa straika kutokana na Arouna Kone kuwa mgonjwa, Martinez hana chaguo jingine zaidi ya kuingia sokoni na Fabio Quagliarella wa Juventus ndiye mtu anayemhitaji.
Wenger amechoshwa na Oliver Giroud na hivyo anawatazama zaidi Higuain na Falcao, sawa na Mourinho alivyochoshwa na mastraika wake watatu ambao hawana maana yoyote kwenye ligi hadi sasa.
Kocha mpya wa Tottenham, Tim Sherwood hatakuwa na uwezo wa kumgharimia Higuain, lakini tayari atakuwa na Pauni 20 Milioni kwa ajili ya kumnasa straika mpya sawa na Brendan Rodgers wa Liverpool, ambaye atahitaji kuongeza mtu mwingine wa maana ili kupunguza utegemezi kwa Luis Suarez and Daniel Sturridge.
Kwenye nafasi za chini katika msimamo, kocha wa Crystal Palace, Tony Pulis anataka mastraika wawili kukinusuru kikosi hicho kinachougua ugonjwa wa mabao.
Stoke City nao wamekuwa wakisuasua kwenye ufungaji na hilo litamfanya Mark Hughes kuingia sokoni. Kutokana na Andy Carroll kuwa majeruhi, West Ham inahitaji kupata straika mpya mwezi ujao jambo ambalo linaweza kushuhudia pesa nyingi sana zikitumika kwenye usajili wa Januari kwa klabu hizo za Ligi Kuu England.
Mwaka 2011, kwenye usajili wa Januari klabu za Ligi Kuu England zilishuhudia zikitumika Pauni 85 milioni kwa wachezaji wawili tu, Andy Carroll alipotua Liverpool na Fernando Torres alipotimkia Chelsea kwa Pauni 50 milioni. Kiwango hicho kilikuwa kikubwa sana kwenye usajili kwa Januari pekee, lakini msimu huu mambo yanaweza kuwa tofauti zaidi kutokana na klabu nyingi kuhitaji mastraika, wachezaji ambao wanaaminika kuwa ghali zaidi kwenye soko la usajili wa wachezaji.
Share on Google Plus

About feisal pinto

Computer Application Student, Author, Short Stories Writer, Business Proposal Writer, Presenter and Application Builder. Email feisalpinto4@gmail.com for complains and business only.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment

ad