.

.

SHOP HERE

News
Loading...

.

.

.

shop now

Matajiri Yanga wavamia kambi ya Al-Ahly Cairo

Wachezaji wa timu ya Yanga wakishangilia ushindi wa bao moja dhidi ya timu ya Al-Ahly ya Misri
MATAJIRI wawili wenye ushawishi mkubwa na wanaofanya mambo mengi ya Yanga, hawajaridhika na ushindi wa juzi Jumamosi wa bao 1-0 dhidi ya Al Ahly na sasa wameamua kuivalia njuga klabu hiyo ya Misri kwa kuvamia mji wao wa Cairo ili kuweka mambo sawa kabla ya mechi ya marudiano ya Jumapili.
Wakati jopo la Yanga lilitangulia kuwasili Cairo jana Jumapili  kudhibiti mbinu za Waarabu hao na kuhakikisha hakuna fitna yoyote itakayofanyika, wenyeji wao walikuwa nchini ambapo jioni walifanya mazoezi yao ya mwisho na baadaye kula chakula cha usiku na maofisa wa ubalozi wao nchini na wataondoka leo Jumatatu.
Matajiri hao ambao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Abdallah Binkleb na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Kimataifa, Seif Ahmed wamewaongoza wanachama wengine kuingia msituni kuidhibiti Ahly kwa ushirikiano na Watanzania wanaoishi jijini Cairo, Misri.
Seif aliondoka nchini kimyakimya na akaliambia Mwanaspoti kwamba wamepania kuiondosha Ahly na wanachokwenda kufanya ni kuhakikisha Wachezaji wa Yanga wanakuwa chini ya uangalizi mkali katika kila dakika tangu watakapotua kwenye Uwanja wa Ndege Alhamisi wiki hii.
Seif alisisitiza kuwa walishaanza kuweka mazingira mapema, lakini sasa wanakwenda kujidhatiti zaidi kuanzia kwenye Uwanja wa kufanyia mazoezi, hoteli, mabasi pamoja na vyakula kwani hawataki kutumia kitu chochote cha wenyeji ili kuepuka hujuma kwenye mechi hiyo itakayochezwa Jumapili usiku.
“Tumepata ushindi wa kihistoria lakini hatuwezi kukaa chini kushangilia, kwa sasa tunatakiwa kuanza maandalizi ya mechi ya marudiano ndio maana naondoka kuelekea Misri kufanya mambo,” alisisitiza Seif.
“Tunatakiwa kujipanga vizuri kabla ya mchezo wa marudiano, kabla ya timu kufika kuna mambo ambayo ni lazima tuyaweke sawa ili kukamilisha lengo letu la kusonga mbele, kuna haja ya kuandaa sehemu salama ya kufikia kikosi chetu, wapi tutafanyia mazoezi ni lazima tuyafanye hayo yote sasa, hawa jamaa inabidi kuwa nao makini sana.”
Akizungumza na Mwanaspoti, Abdallah Bin Kleb alisema: “Tunajua wenzetu watakuwa wamejiandaa kuhakikisha wanatufunga nyumbani kwao, hivyo tumeanza maandalizi rasmi katika kuhakikisha tunapata ushindi ugenini baada ya kuwafunga nyumbani.
“Kiongozi mmoja anatangulia Misri, timu inaondoka Alhamisi na kufika Ijumaa, itachelewa kuondoka kutokana na mechi hiyo kuchezwa Jumapili.”
Kocha Al Ahly aitisha
Kocha Mkuu wa Al Ahly, Mohamed Youssef, amesema kuwa hatakubali kufungwa mara mbili na Yanga, ugenini na nyumbani.
“Nimeziona mbinu za wapinzani wangu Yanga, sina hofu ya mechi ya marudiano tutakayorudiana na wapinzani wetu, nimepanga kwenda kukiboresha kikosi changu ili mechi ya marudiano tushinde,” alisema.
“Yanga ni timu nzuri yenye wachezaji wazuri, lakini hilo haliniogopeshi kabisa, bado tunayo nafasi kutokana na wapinzani wetu kutufunga bao moja tu, nina matumaini makubwa ya kushinda mechi hiyo.”
Kocha Yanga kushambulia
Kocha Mholanzi wa Yanga, Hans Van Der Pluijm, amesema: “Tumeshinda nyumbani lakini bado tuna mechi ya marudiano na tutakuwa kwao ambako wana sifa moja ya kutofungika. Kwa sababu najua mbinu zao, nimejiandaa nao, tunaenda kucheza kwa kushambulia tu bila woga, ushindi huu wa bao 1-0 hauwezi kutudanganya kuwa kule tukazuie tu, haitakuwa hivyo.
“Mnapozuia ni kwamba mmeridhika, lakini sisi tutatafuta ushindi tu, wale jamaa wanapokuwa kwao ndiyo wanakuwa wajanja sana na mbinu nyingi, lakini pamoja na mambo yao yote hayo, hatutawahofia na tutawafunga huko huko kwao.”
Okwi aonya
Emmanuel Okwi, amefurahi kuvunja mwiko kwa kuisadia timu yake kupata ushindi wa bao 1-0 lakini akawashushia onyo zito wachezaji wenzake akiwamo yeye mwenyewe.
“Ukweli ni kwamba kupata ushindi katika mechi ya nyumbani ni jambo ambalo kila mmoja wetu atalifurahia, mechi ilikuwa ngumu lakini sasa ni wakati mimi pamoja na wachezaji wenzangu kuanza kufikiria kuhusu mchezo ujao wa marudiano na kuacha kushangilia huu mchezo wa kwanza,” alisema Okwi.
“Bado tuna dakika 90 nyingine ugenini, ambazo naamini hazitakuwa rahisi kwetu, tunatakiwa kujituma zaidi kama kweli tuna lengo la kusonga mbele, hawa jamaa wanakwenda kujipanga kutukabili na sisi lazima tijiandae kwa kiwango kikubwa.”
Haruna Niyonzima yeye alisema; “Walitumia historia yao kutubeza na kuonekana sisi hatuwezi kitu mbele yao, sasa kila mtu anatuamini na ninakueleza kuna kitu tutafanya na tutatambulika Afrika yote. Nasema lazima tushinde.”
Share on Google Plus

About feisal pinto

Computer Application Student, Author, Short Stories Writer, Business Proposal Writer, Presenter and Application Builder. Email feisalpinto4@gmail.com for complains and business only.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment

ad